Risala kwa wananchi kilele wiki ya maji 2013 bulendabufwe bunda iliyosomwa na eng tanu deule
1. HALMASHAURI YA WILAYA YA BUNDA
RISALA KWA WANANCHI KWENYE MAADHIMISHO YA KILELE CHA WIKI YA MAJI KIWILAYA
TAREHE 22/03/2013 KATIKA KIJIJI CHA BULENDABUFWE
Ndugu Kaimu Afisa Mtendaji wa Kata ya Igundu, Mr Tekele Mligawe
Mheshimiwa Mwenyeviti wa kijiji cha Bulendabufwe
Waheshimiwa Wenyeviti wa vitongoji mliofika hapa
Mhe Mwenyekiti wa kamati ya maji ya mradi wa Bulendabufwe
Ndugu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Bulendabufwe, Mr Mzaga Msekwa
Ndugu waandishi wa habari
Wananchi wa Kijiji cha Bulendabufwe
Mabibi na Mabwana, Tumsifu Yesu Kristo, Asalaam Aleykum
Ndugu Wananchi; Kama ilivyo kawaida, Taifa letu kila mwaka huungana na Mataifa
mengine Duniani katika kuadhimisha sherehe ya wiki ya maji kuanzia tarehe 16 Machi
hadi tarehe 22 Machi kila mwaka.
Kauli Mbiu
Ndugu Wananchi; “Kauli mbiu” ya maadhimisho ya wiki ya maji mwaka huu ni “MWAKA
WA USHIRIKIANO WA MAJI KITAIFA.
Madhumuni ya sherehe
Ndugu Wananchi; madhumuni makuu ya maadhimisho ya sherehe hizi kila mwaka
yamekuwa yakilenga katika kuweka msukumo zaidi katika kuwahamasisha ninyi
wananchi na watumiaji maji wote kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kushiriki katika
kupanga, kujenga, kufanya matengenezo ya miradi yenu na umuhimu wa kutunza vyanzo
vya maji.
Aidha maadhimisho haya yamekuwa yakilenga kuwaelimisha ninyi wananchi kuhusu sera
ya Taifa ya Maji na mikakati inayohusu upatikanaji wa huduma ya maji. Sera hii ya maji ya
2. mwaka 2002 inaweka msisitizo kwa watumiaji maji wenyewe kuchangia gharama za
uendeshaji na matengenezo kwa asilimia 100
Huduma ya Maji Kiwilaya
Ndugu Wananchi; Pamoja na wilaya kuwa na visima vingi vifupi na virefu pia wilaya yetu
ina miradi minane (8) ya maji ya bomba ambayo ni Mradi wa maji wa Iramba,
Bulendabufwe, Kibara, Kasahunga, Bunda mjini, Nyamuswa, Nyaruga na Chamtigiti.
Katika miradi yote hii ya bomba ni miradi ya Bulendafwe, Nyaruga na Chamtigiti pekee
ndiyo haitumii nishati ya aina yoyote ile, yaani maji yanateremka yenyewe kwa wananchi
bila kusukumwa na mitambo. Kwa hivi sasa Wilaya ya Bunda ina asilimia 48 ya watu wake
wanaopata maji safi na salama ndani ya umbali unaokubalika kisera yaani umbali usiozidi
mita 400. Kwa hapa Bulendabfwe, Mradi huu wa maji mtiririko ulikuwa unahudumia
asilimia 80 ya wakazi wote japo kwasasa chanzo chake cha maji kimeharibika na bomba
kuu la kuteremsha maji limepasuka.
Matatizo ya mradi huu kwa ujumla wake:-
(i) Chanzo kimeharibiwa na watu waliochimba malambo ya kunyweshea mifugo
(ii) Mifugo inayofika kunywa maji inaendelea kuharibu chanzo cha maji.
(iii) Watu wanalima mashamba kwenye eneo la chanzo cha maji na kusababisha
mmomonyoko wa udongo unaoziba macho ya chanzo cha maji
(iv) Madawa ya kilimo cha pamba na mazao mengine yanachangia kuharibu ubora
wa maji kwa matumizi ya majumbani.
(v) Watu wanaoishi na kufanya shughuli za kibinadamu kwenye chanzo kama vile,
kuchimba na kutumia vyoo vya shimo wanahatarisha usalama wa maji
Madhara yatokanayo na Uharibifu wa Vyanzo vya maji
(i) Watu kunywa maji yaliyo na madawa kama vile dawa za pamba, mbolea, n.k
(ii) Watu kunywa maji yenye kinyesi cha wanyama na kinyesi cha binadamu.
(iii) Uoto wa asili unapoondoka, maji machafu yanaingia bila kuchujwa na uoto huo
Mikakati ya kunusuru chanzo hiki cha Maji
Ndugu Wananchi; Kwa kuwa sera ya maji ya mwaka 2002 inasisitiza watumiaji maji
wenyewe kuhusika kwa asilimia 100 katika kuendesha na kutengeneza miradi yao ya
maji, hivyo mambo yafuatayo yanapaswa yafanyike ili kunusuru mradi huu wa maji:-
3. Malambo yaliyochimbwa kwenye chanzo cha maji yanatakiwa yafukiwe.
Wakulima waache kabisa kulima eneo la juu ya chanzo na wapewe eneo mbadala.
Wakazi wanaoishi juu ya chanzo wahamishwe na kupewa makazi mengine.
Watu wasichome moto, wala wasikate miti ovyo na wasitengeneze mkaa.
Wananchi waanzishe mfuko wa fedha za uendeshaji na matengenezo ya mradi
Mifugo ya aina yoyote isiruhusiwe kabisa kufika kwenye chanzo cha maji.
Chanzo cha maji kizungushiwe wigo wa miti, Mikonge au fensi ya waya wa chuma.
Wananchi wapande miti inayohifadhi maji kwenye eneo la chanzo cha maji.
Ndugu Wananchi; Sambamba na mikakati hiyo hapo juu, kwa kuwa “Kauli mbiu” ya wiki
ya maji Duniani kwa mwaka huu inasema MWAKA WA USHIRIKIANO WA MAJI KITAIFA,
hivyo napenda kumshukuru Mhe Mkuu wa wilaya kwa jitihada zake mbalimbali za
kunusuru chanzo hiki cha maji na pia niwashukuru wananchi waliochanga fedha za
kufanya ukarabati huu. Sisi watumishi pia tumekuwa mstari wa mbele kutoa utaalamu
wetu na ueledi katika masuala haya ya sera na miundombinu ya maji na ndiyo maana
watumishi wa Idara ya maji leo wamefika hapa kwenye chanzo cha maji kufanya
ukarabati wa bomba lililoharibika. Sas kwa kuwa kauli mbiu yetu tumeanza kuitekeleza
kwa vitendo hivyo naomba ushirikiano uendeleee kati ya wananchi wote wakulima kwa
wafanyakazi, wanasiasa na watumishi wa umma na pia kwa wadau mbalimbali ili kulinda
maji yetu yatufae sisi leo na vizazi vijavyo hapo siku za baadaye.
Maji ni Uhai na Usafi wa mazingira ni utu
Siku ya maji duniani Hoyeee
SIku ya maji kiwilaya Hoyeeee
Eng. Tanu Deule
MHANDISI WA MAJI (W) YA BUNDA.